NANI ATACHEZA NA NANI ROBO FAINALI YA COPA AMERICA…RATIBA HII HAPA.
Robo fainali ya kwanza
itawakutanisha wenyeji wa michuano hiyo timu ya Chile itakuwa ikikipiga
dhidi ya Uruguay siku ya Jumatano, Chile watahitaji ushindi kwa nguvu
zote kwasababu wao ndio wenyeji wa michuano hivyo watataka kuhakikisha
wanafika mbali kwenye mashindano hayo wakiwa kwenye ardhi ya nyumbani
wakiongozwa na nyota wao wa Arsenal Alexis Sanchez na kiungo wa Juventus
Aturo Vidal.
Lakini Cavani, Godin na nyota
wengine wengi wa Uruguay watakuwa tayari kuwakabili Chile kwenye mchezo
huo wa robo fainali ya kwanza.
Bolivia wao watakipiga dhidi ya
Peru kwenye robo fainali ya pili itayochezwa siku ya Alhamisi. Bolivia
imewashangaza wengi kwa kutinga kwake hatua ya robo fainali kwasababu
wengi walikuwa wakiibeza na kutoipa nafasi kwenye michuano ya mwaka huu.
Lakini mshambuliaji wa Bayern Munich Claudio Pizarro anatarajiwa
kukiongoza kikosi cha Peru kuikabili Bolivia.
Mchezo mwingine utakaovuta hisia
za watu wengi ni ule ambao Argentina itakapochuana na Colombia kwenye
robo fainali ngumu na ya kukata na shoka itakayopigwa siku ya Ijumaa.
Nyota wa klabu ya Barcelona
Lionel Messi atakuwa akiwaongoza nyota wengine kama Di Maria, Aguero,
Tevez na wengine wengi kutafuta ushindi mbele ya Colombia ambayo
inaongozwa na nyota wa Madrid James Rodriguez na wenzake kama Cuadrado
na Falcao.
Brazil watakipiga dhidi ya
Paraguay kwenye robo fainali ya mwisho itakayochezwa Jumamosi. Brazil
bado itaendelea kumkosa Neymar na itakuwa ikitupa karata yake ya pili
kujaribu kutafuta ushindi bila nyota huyo aliyefungiwa mechi nne.
Ratiba kamili ya robo fainali hii hapa;
Chile v Uruguay – Jumatano
Bolivia v Peru – Alhamisi
Argentina v Colombia – Ijumaa
Brazil v Paraguay – Jumamosi